Thursday, August 25, 2011

MHESHIMIWA NI NANI?

Rais mheshimiwa,Makamu mheshimiwa
waziri mheshimiwa,naibu mheshimiwa,
spika mheshimiwa,katibu mheshimiwa,
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?

Mimi ni mkata miwa,hivi si mheshimiwa?
kutwa nakatwa na miwa,pesa kichele napewa,
na hao waheshimiwa ,kila kitu wanapewa
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?,


Hakimu mheshimiwa,wakili mheshimiwa,
wada ni mheshimiwa,afande mheshimiwa,
diwani mheshimiwa,balozi mheshimiwa,
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?
 
Mhudumu ofisini,siitwi mheshimiwa,
mpika chai shuleni,siitwi mheshimiwa,
msafishaji chooni,siitwi mheshimiwa,
  Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?

Padri mheshimiwa,Shehe ni mheshimiwa,
mbunge  mheshimiwa,mjumbe mheshimiwa,
tajiri mheshimiwa,fukara alaumiwa,
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?

Mimi nalima shambani,siitwi mheshimiwa,
navuta mkokoteni,siitwi mheshimiwa,
nesi hospitalini,siitwi,mheshimiwa,
  Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?


Huyu mkuu wa shule,aitwa mheshimiwa,
rafiki badi Bakule,haitwi mheshimiwa,
bwana kaka kando kule,wewe ni mheshimiwa,
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?

Mgonjwa hospitali,haitwi mheshimiwa,
mwenye nzuri yake hali,haitwi mheshimiwa,
mwenye kuchunga fahali,haitwi mheshimiwa,
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?

Mambo mnayaharibu,eti ni waheshimiwa,
mnajitia mabubu,maswali mkitupiwa,
matatizo yatusibu,porojo zenu twalewa,
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?

Konisaga nashangaa,wapi tunaelekea,
neno ndugu lapotea,gizani latokomea,
hakika tulizoea,udugu liliulea,
 Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?

Sasa ninamalizia,neno hilo silipendi,
sana laleta udhia,latuletea makundi
 usawa utapotea,sawa wa njiwa na bundi,
  Hili linanichanganya,nani ni mheshimiwa?






































,



Wednesday, August 24, 2011

SWALA TUMETEGA WOTE

Tu wawindaji pamoja,porini tumeingia,
sote tumejenga hoja,wanyama kujipatia,
hata sungura akija,sawa tutajigawia,
 Swala tumetega wote,vipi ule peke yako?

windoni tulipotega,macho tukayapanua,
walisogolea mbega,balaa kutuletea,
tukajifunga lubega,mbali kuwafukuzia,
 Swala tumetegaa wote vipi ule peke yako?

Twajua wewe mkubwa,kati yetu wawindaji,
hata kuwinda kwa mbwa,kelele utahitaji,
huwezi ruka kwa mbwa,hunacho hicho kipaji,
 Swala tumetega wote,vipi ule peke yako?

Tulipoanza usasi,umoja tuliujenga,
hatukuwa na risasi,marungu tuliyatenga,
hakutokea muasi,kati kulileta janga,
 Swala tumetega wote,vipi ule peke yako?

Tulijipangia zamu,kwenda kuona mitego,
tena kwa mashamushamu,tulikwenda kwa mikogo,
nasi hatukufahamu,kumbe kuna mikorogo,
 Swala tumetega wote,vipi ule peke yako?

Swala alipotegeka,ilikuwa zamu yako,
begani ukamuweka,haraka chumbani kwako,
chini ukajibweteka,umezua sokomoko,
  Swala tumetega wote,vipi ule peke yako?

Msiri ulomwambia,yeye hajui kuchuna,
kisu atakupatia,swala mpate kuchuna,
uchoyo umekujia,hasidi lako ni jina,
  Swala tumetega wote,vipi ule peke yako?



































Tuesday, August 23, 2011

KIFUNGUA MACHO

SHAIRI LA SALAMU.
Uanze kwa kufikiri,unapotunga shairi,
kuyapanga mashairi,yapasa uwe mahiri,
kuifikisha habari,ni kazi kweli si siri,
 Hatutaki ufahari,ushairi ni safari.