Tunapotafuta kazi,heshima tunaonyesha,
kwamba tumepata kozi,na vyeti kuvionesha,
vyeti vyetu si vya wizi,hili tunadhihirisha
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Ulishindia viazi,kutwa kucha ulikesha,
hukufanya upuuzi,muda wako ulitosha,
hayo uliyamaizi,wazembe walikupisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Sasa umepata kazi,umeanza kutuchosha,
umeanza udowezi,hivi sasa nakupasha,
kwa bosi mchokonozi,tamaa inakuwasha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Wewe ni msaidizi,vyombo kwetu unaosha,
wapi ulipata kozi,waanza tugombanisha,
tuko kama wakimbizi,chuki twajibebanisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Sasa tumekuwa nazi,vichwa watugonganisha,
hivi tumejua wazi,umbea unakuwasha,
huyawezi maamuzi,kila jambo wapotosha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
wewe ni kama mkwezi,majungu kuyapandisha,
kazi yako upakuzi,fitina kufurumusha,
hauishi uchakuzi,tabia yako yatisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Kazi wewe hauwezi,sote tumebainisha,
fitina ni muenezi,cheo unajipand isha,
sasa muombe mwenyezi, mbinguni kukufikisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Tabia kama ya mbuzi,mapembe umepandisha,
mabawa kama nyambizi,nani akupe motisha,
acha wako upekuzi,ziwani tutakurusha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Kusema yote siwezi,nimekwisha kujulisha,
nakwambia simalizi,beti nyingi zinatosha,
usipatwe jinamizi,nani ataja lishusha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Mimi si king'ang'anizi,polepole najishusha,
sijatoa simulizi,ya moyoni nimeshusha,
nimekwisha kubarizi,kazi nakupa Elisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?
Konisaga Mwafongo 0717248828
No comments:
Post a Comment