Wengi twapenda tembea,maeneo mbalimbali,
wazo linapokujia,tena kama una hali,
utakachofikiria,kwenda popote mahali,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
Ndege ulotegemea,sasa imefika mbali,
kwako kilichobakia,hali yako ni muhali,
punguza kufikiria,endelea saka mali,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine
ndege uliyozoea,imekuwa bei kali,
siti ulizokalia,kwako sasa bei ghali,
zile nilikukatia,kwako tena si halali,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
Kote tulikotembea,hata visiwa vya Bali,
uliona mazoea,gharama hukuzijali,
kutwa ulijidekea,kumshinda hata mwali,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
Jinsi nilikutendea,mimi wa Mungu mjoli,
uliona mchekea,ukajifanya mkali,
tiketi kunitupia,kusema si mali kitu,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
Hata basi safiria,hiyo ndiyo yako mali,
ndege acha fikiria,kwa yake hayo makali,
yasahau mazoea,sasa nakupa ukweli,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
Mangapi nitongea,hayabadili ukweli,
kutwa nikisimulia,ukweli sitabadili,
kitu kilichobakia,vumilia kama soli,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
Vipi nikihadithia,sitabadili ukweli,
machozi nikiyatoa,sitobadili kauli,
wengi watanishangaa,jitu hili ni katili,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
mimi nilifikiria,una pungufu nauli,
kumbe mi nilichelea,huna hata ya ugali,
kama mboga yapelea,ongeza na pilipili,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
Ushauri ninatoa,uspunguze kusali,
nauli kujipatia, walau basi la pili,
ushauri zingatia pia muombe Jalali,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.
No comments:
Post a Comment