Washairi nauliza,jibu nipeni yakini,
swali limeniumiza,jibu sijalibaini,
uchunguzi wanikwaza,jibu waweka sirini,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Soko lilipoungua,mengi mlitueleza,
kamanda aelezea,chanzo bado chatatiza,
sisi tunasubiria,wao nini wanawaza,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Jambazi amekamatwa,vyombo vyote mwatangaza,
hakika alipopatwa,sana tulijiliwaza,
hakuna aliyesutwa,sasa twaona mwangaza,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Wizi wa mali ya umma,mwauripoti kwa kina,
utadhani huko nyuma,hamkupata uona,
magazeti tunasoma,runingani tunaona,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
kakamatwa muuaji,aliyewaua wengi,
mambo mengi hamtaji,aliuza hata bangi,
aliuvuruga mji,sasa miji hatafungi,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
wanaotupa vichanga,wahitaji uchunguzi?
tunaowaita wanga,ni wa nini uchunguzi,
porojo mnazipanga huo sasa upuuzi,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Tairi limepasuka,ajali ikatokea,
hakuna aliyesuka,limekuwa kama baa,
mioyo inashituka,maisha yanapotea,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Huo wenu uchunguzi,mimi ninauchukia,
unatupa usingizi,kwa tunavyosubiria,
imekuwa upuuzi,nini kinaendelea,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Mimi sijapata soma,majibu ya uchunguzi,
labda mliosoma,mwaniona mchochezi,
sasa nasimama hima,mimi si mchokonozi,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Namaliza kwa kusema,uchunguzi endelea,
umeshachoka kusoma,uchunguzi fatilia,
hapa mimi ninakoma,hivi sasa nasinzia,
Hivi huo uchunguzi,majibu mwatupa lini?
Konisaga Mwafongo 0717248828