Tuesday, December 8, 2015

KUMBE INAWEZEKANA

Kumbe inawezekana,Rais akiamua,
hakunaatayekana,agizokupuuzia,
usafi ulivyofana,sote tuanfurahia,
 Leosikuya Uhuru,kazitumefanikisha.

Bajeti alivyobana,wanyonge twafurahia,
ameiondoa dhana,mabosi pesa jilia,
angalau twafanana,wote tunacheklea,
  Leo siku ya uhuru,kazi tumefanikisha.

Konisaga@gmail.com
0717 24 88 28//0629902077
09/12/2015
 

Tuesday, November 5, 2013

RAFIKI HUTOMJUA



Kupata mwema rafiki,sala yapasa shiriki,
Wako wengi wanafiki,tena vinara wa chuki,
Jaribu kumhakiki,Mola akupe a haki,
  Rafiki hutomjua,asilani abadani.

Rafiki mfano nyuki,utaishia mikuki,
Atakujaliza dhiki,na kukujaza mikiki,
Hutoipata riziki,kwa rafiki alo “shirki”,
    Rafiki hutomjua,asilani abadani.

Wengi wao wazandiki,shida hawatoshiriki,
Misibani hawatoki,kukung’ong’a watabaki,
Utabaki kuhamaki,furaha hutomiliki,
    Rafiki hutomjua,asilani abadani


Konisaga  Mwafongo-0717 248828/0767 24 88 28 Mbeya.

TUMEPOTEA



Nyuma nikiangalia,hakika tumepotea,
Mbele nikiangalia,jua lazidi kuchwea,
Twapoteza asilia,vya wageni twapokea,
    Sio kila cha mgeni,yatupasa kupokea.

Ngoma za kiasilia,hebu sasa angalia,
Haziwezi kuvutia,walisha tuharibia,
Midundo tulosifia,sasa ni historia,
Sio kila cha mgeni,yatupasa kupokea.

Ukarimu angalia,sivyo tulivyozoea,
Usasa umetukaa,ubize twasingizia,
Udugu “ulishapaa”,tumebaki kuduwaa,
Sio kila cha mgeni,yatupasa kupokea.

Kwa jirani kutembea,sasa waitwa umbea,
Wataka hali Julia,eti unawasumbua,
Simu ungewapigia,mbona wangeipokea,
Sio kila cha mgeni,yatupasa kupokea.

Mola ametujalia,mlo wetu asilia,
Sasa kilichoingia,hakika waweza lia,
Makapi watupatia,uleo wasingizia,
Sio kila cha mgeni,yatupasa kupokea.

Gharama twajiletea,mazishini angalia,
Mapesa tunayatoa,na sare kuandalia,
Tungeweza kujitoa,uhai hangaikia,
Sio kila cha mgeni,yatupasa kupokea.

SHAIRI GUMU LA NINI?



Mashairi burudani,pale unapoyasoma,
Shairi gumu la nini,ni nini unachopima,
Halikai akilini,kando utalisukuma,
  Shairi gumu la nini,halileti burudani.

Yasome magazetini,kweli kichwa kitauma,
Unaweza ukadhani,kaandika kisukuma,
Kama si cha upareni,basi lugha ya Musoma,
  Shairi gumu la nini,halileti burudani.

Ufikapo vibandani,gazeti ukalifuma,
Utafurahi moyoni,na tena utajituma,
Pesa ipo mfukoni,nyumbani nitalisoma,
  Shairi gumu la nini,halileti burudani.

Soma kilichomo ndani,shairi hutolisoma,
Wajigeuza kitini,kweli leo unakoma,
Sio tena burudani,masikio yanavuma,
  Shairi gumu la nini,halileti burudani.

Mashairi kweli fani,wengi twapenda yasoma,
Washairi andikeni,tutayoweza kusoma,
Unamkomoa nani,Konisaga ninasema,
  Shairi gumu la nini,halileti burudani.

Konisaga  Mwafongo-Mbeya  0717 24 88 28/0767 24 88 28

Tuesday, May 28, 2013

NENO "KAMA" LACHANGANYA


NENO “KAMA”LACHANGANYA.
Neno “kama” kweli  gumu,kulitumia vigumu,
Kama wasoma isimu,tupunguzie ugumu,
Lugha si mwanaharamu,nayo inayo rasimu,
  Neno “kama”lachanganya,jamani tuwe makini.

Mimi “kama’ ni mwalimu,wiki hii niko zamu,
Nikikukuta sehemu,usije kunilaumu,
Mwalimu ulihitimu,”kama”hapo si sehemu,
    Neno “kama”lachanganya,jamani tuwe makini

Mheshimiwa hakimu,kazi yako kweli ngumu,
Unaposoma hukumu,roho kweli iwe ngumu,
Na mimi “kama” hakimu,mvua sita kazi ngumu,
  Neno “kama”lachanganya,jamani tuwe makini 

Mimi “kama”mhudumu,faili zamu kwa zamu,
Wote muwe na nidhamu,nisjie panda wazimu,
Kazi yangu mfahamu,ni ngumu msilaumu,
  Neno “kama”lachanganya,jamani tuwe makini

N a mimi “kama”Adamu,nimemzaa Swaumu,
Mtoto wangu wa damu,Mola amenirehemu,
Nitampenda dawamu,kama mwana wa Kikwemu,
  Neno “kama”lachanganya,jamani tuwe makini

Mbunge wetu udumu,hii ni yako awamu,
Watu wako tuna hamu,tatua kero kwa zamu,
Na mimi “kama”mwalimu,kusema siishi hamu,
  Neno “kama” kwa hakika,hapo  ni mahala pake.

Viongozi silaumu,neon hilo kwenu gumu,
Mwatushushia “mabomu”,najua hamfahamu,
Mbona mkijaza fomu,huwa mnalifahamu,
    Neno “kama”lachanganya,jamani tuwe makini  

Naweka chini kalamu,neno “kama”lifahamu,
Sio kuwa nashutumu,neno “kama”sina hamu,
Ninawaomba walimu ,lirudisheni utamu,
     Neno “kama”lachanganya,jamani tuwe makini
Konisaga Mwafongo
Simu:0717  24 88 28

Wednesday, February 13, 2013

NDEGE IMESHAONDOKA

Wengi twapenda tembea,maeneo mbalimbali,
wazo linapokujia,tena kama una hali,
utakachofikiria,kwenda popote mahali,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

Ndege ulotegemea,sasa imefika mbali,
kwako kilichobakia,hali yako ni muhali,
punguza kufikiria,endelea saka mali,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine


ndege uliyozoea,imekuwa bei kali,
siti ulizokalia,kwako sasa bei ghali,
zile nilikukatia,kwako tena si halali,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

Kote tulikotembea,hata visiwa vya Bali,
uliona mazoea,gharama hukuzijali,
kutwa ulijidekea,kumshinda hata mwali,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

Jinsi nilikutendea,mimi wa Mungu mjoli,
uliona mchekea,ukajifanya mkali,
tiketi kunitupia,kusema si mali kitu,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

Hata basi safiria,hiyo ndiyo yako mali,
ndege acha fikiria,kwa yake hayo makali,
yasahau mazoea,sasa nakupa ukweli,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

Mangapi nitongea,hayabadili ukweli,
kutwa nikisimulia,ukweli sitabadili,
kitu kilichobakia,vumilia kama soli,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

Vipi nikihadithia,sitabadili ukweli,
machozi nikiyatoa,sitobadili kauli,
wengi watanishangaa,jitu hili ni katili,
Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

mimi nilifikiria,una pungufu nauli,
kumbe mi nilichelea,huna hata ya ugali,
kama mboga yapelea,ongeza na pilipili,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.

Ushauri ninatoa,uspunguze kusali,
nauli kujipatia, walau basi la pili,
ushauri zingatia pia muombe Jalali,
  Ndege imeshaondoka,kata tiketi nyingine.


















NI KWELI WATAKA KAZI?

Tunapotafuta kazi,heshima tunaonyesha,
kwamba tumepata kozi,na vyeti kuvionesha,
vyeti vyetu si vya wizi,hili tunadhihirisha
  Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Ulishindia viazi,kutwa kucha ulikesha,
hukufanya upuuzi,muda wako ulitosha,
hayo uliyamaizi,wazembe walikupisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Sasa umepata kazi,umeanza kutuchosha,
umeanza udowezi,hivi sasa nakupasha,
kwa bosi mchokonozi,tamaa inakuwasha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Wewe ni msaidizi,vyombo kwetu unaosha,
wapi ulipata kozi,waanza tugombanisha,
tuko kama wakimbizi,chuki twajibebanisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Sasa tumekuwa nazi,vichwa watugonganisha,
hivi tumejua wazi,umbea unakuwasha,
huyawezi maamuzi,kila jambo wapotosha,
  Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

wewe ni kama mkwezi,majungu kuyapandisha,
kazi yako upakuzi,fitina kufurumusha,
hauishi uchakuzi,tabia yako yatisha,
  Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Kazi wewe hauwezi,sote tumebainisha,
fitina ni muenezi,cheo unajipand isha,
sasa muombe mwenyezi, mbinguni kukufikisha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Tabia kama ya mbuzi,mapembe umepandisha,
mabawa kama nyambizi,nani akupe motisha,
acha wako upekuzi,ziwani tutakurusha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Kusema yote siwezi,nimekwisha kujulisha,
nakwambia simalizi,beti nyingi zinatosha,
usipatwe jinamizi,nani ataja lishusha,
Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?

Mimi si king'ang'anizi,polepole najishusha,
sijatoa simulizi,ya moyoni nimeshusha,
nimekwisha kubarizi,kazi nakupa Elisha,
  Ni kweli wataka kazi au wataka kingine?


Konisaga Mwafongo 0717248828